Ezekiel 19

Maombolezo Kwa Ajili Ya Wakuu Wa Israeli

1 a“Wewe fanya maombolezo kuhusu wakuu wa Israeli 2 bna useme: “ ‘Tazama jinsi gani mama yako alivyokuwa simba jike
miongoni mwa simba!
Alilala katikati ya wana simba
na kulisha watoto wake.

3 cAlimlea mmoja wa watoto wake,
naye akawa simba mwenye nguvu.
Akajifunza kurarua mawindo
naye akala watu.

4 dMataifa wakasikia habari zake,
naye akanaswa katika shimo lao.
Wakamwongoza kwa ndoana
mpaka nchi ya Misri.


5 e“ ‘Mama yake alipongoja na kuona tumaini lake halitimiziki,
nayo matarajio yake yametoweka,
akamchukua mwanawe mwingine
na kumfanya simba mwenye nguvu.

6 fAlizungukazunguka miongoni mwa simba,
kwa kuwa sasa alikuwa simba mwenye nguvu.
Akajifunza kurarua mawindo
naye akala watu.

7 gAkabomoa ngome zao
na kuiharibu miji yao.
Nchi na wote waliokuwa ndani yake
wakatiwa hofu kwa kunguruma kwake.

8 hKisha mataifa wakaja dhidi yake
kutoka sehemu zilizomzunguka.
Wakatanda nyavu zao kwa ajili yake,
naye akanaswa katika shimo lao.

9 iKwa kutumia ndoana wakamvutia kwenye tundu
na kumleta mpaka kwa mfalme wa Babeli.
Wakamtia gerezani, hivyo kunguruma kwake
hakukusikika tena
katika milima ya Israeli.


10 j“ ‘Mama yako alikuwa kama mzabibu
katika shamba lako la mizabibu
uliopandwa kando ya maji,
ukiwa unazaa sana na wenye matawi mengi
kwa sababu ya wingi wa maji.

11 kMatawi yake yalikuwa na nguvu,
yaliyofaa kuwa fimbo ya enzi ya mtawala.
Ulikuwa mrefu kupita miti mingine
katikati ya matawi manene;
ulionekana kwa urahisi
kwa ajili ya urefu wake
na wingi wa matawi yake.

12 lLakini uling’olewa kwa hasira kali
na kutupwa chini.
Upepo wa mashariki uliufanya usinyae,
matunda yake yakapukutika,
matawi yake yenye nguvu yakanyauka
na moto ukayateketeza.

13 mSasa umepandwa jangwani
katika nchi kame na ya kiu.

14 nMoto ulienea kuanzia katika mmojawapo ya matawi yake makubwa
na kuteketeza matunda yake.
Hakuna tawi lenye nguvu lililobaki juu yake
lifaalo kuwa fimbo ya enzi ya mtawala.’

Hili ndilo ombolezo, na litumike kama ombolezo.”
Copyright information for SwhKC